TAARIFA YA MKOA WA RUKWA YA MAFANIKIO YA MIAKA 50 YA UHURU (DISEMBA 1961 HADI 2011).

 

1.0     UTANGULIZI.

Mkoa wa Rukwa upo Kusini Magharibi mwa Tanzania. Ulianzishwa mwaka 1974 kwa kumega Wilaya ya Sumbawanga kutoka Mkoa wa Mbeya na Wilaya ya Mpanda kutoka sehemu ya Mkoa wa Tabora. Mwaka 1979 Wilaya ya Nkasi ilianzishwa, hivyo Mkoa ukawa na Wilaya tatu Tarafa 21, Kata 79 na Vijiji 372. Mkoa una eneo la km. za mraba 75,250. Kati ya hizo km. za mraba 68,645 ni za nchi kavu na km. za mraba 6,605 ni za maji.

Kulingana na Sensa ya watu na makazi iliyofanyika mwaka 1988 mkoa wa Rukwa ulikuwa na jumla ya watu 703,050 ambalo ni ongezeko la 4.5%, lakini sensa ya watu na makazi iliyofanyika Agosti, 2002 wakazi wa mkoa wa Rukwa walikuwa wameongezeka hadi 1,136,354. Mwaka 2011 Mkoa unakisiwa kuwa na wakazi 1, 558,200 ambalo ni ongezeko la asilimia 3.6% kwa mwaka.  Mkoa huu unapakana na Mikoa ya Tabora, Kigoma na Mbeya. Aidha unapakana na nchi za Zambia na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

 

UMBILE LA MKOA WA RUKWA KWA KIFUPI.

Kabla ya mabadiliko yaliyofanywa na Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mwezi June 2010, Mkoa ulikuwa na Wilaya 3, Majimbo 7 ya Uchaguzi, Halmashauri 5, Tarafa 21, Kata 88, Vijiji 379 na Mitaa 134.

 

HALI YA ULINZI NA USALAMA.

Kwa kipindi cha Miaka 50 hali ya Ulinzi na Usalama katika mkoa ni shwari na ya kuridhishwa kwa kiasi kikubwa. Mtukio machache ya uhalifu yanayojitokeza yameendelea kushughulikiwa na kudhibitiwa na Kamati za Ulinza na Usalama za kila Wilaya kwa kushirikiana na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa.

Matukio haya ni katika maeneo ya Mwambao wa Ziwa Tanganyika. Kwa namna ya pekee tunashukuru sana uwepo wa vikosi viteule vya Jeshi la wananchi katika Vijiji vya Kirando, Kasanga na Ikola ambavyo vinafanya kazi nzuri sana ambayo imesaidia kupunguza matukio ya uvamizi katika Mwambao wa Ziwa Tanganyika. Tunashukuru pia kwa jitihada za JWTZ kuonyesha nia ya kujenga kikosi cha JWTZ Wilaya ya Nkasi wananchi wa Mkoa wa Rukwa wanaimani kuwa uwepo wa kikosi utaimarisha zaidi Ulinzi na Usalama wa maeneo mbalimbali ya Mkoa.

 

HALI YA KISIASA

     Baada ya Uhuru wa Tanganyika mwaka 1961 mkoa ulikuwa unaongozwa na chama kimoja cha siasa kilichojulikana kwa jina la TANU, Mwaka 1977 chama hiki kiliungana na chama cha ASP- cha Zanzibar na kuunda Chama Cha Mapinduzi.  Mwaka 1992 ulianzishwa mfumo wa vyama vingi nchini mpaka mwaka 2011 vyama vya siasa vilivyopo mkoani Rukwa ni Chama Cha Mapinduzi (CCM), Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Chama cha Wananchi (CUF), Chama cha Demokrasia (DP), NCCR-MAGEUZI, UDP na TLP.

 

 SHUGHULI ZA KIUCHUMI NA PATO LA MKOA WA RUKWA KWA  KIFUPI.

Kiuchumi, wakazi wa mkoa wa Rukwa wanajishughulisha na ufugaji, kilimo cha mazao ya chakula na biashara, sekta ya utalii, madini, uvuvi, viwanda  vidogo pamoja na biashara ndogondogo. Pato la Mkoa limekuwa likiongezeka mwaka hadi mwaka, kutoka kiwango cha 3.5% mwaka 1999 hadi kufikia 3.7% mwaka 2004. Kuhusu pato la mwananchi, nalo pia limekuwa likiongezeka kutoka shilingi 239,943 mwaka 1999 hadi kufika Shilingi 369,993 mwaka 2004, na takwimu za mwisho za mwaka 2007 wastani wa pato la Mkoa ulikadiriwa kuwa Shilingi 486,832 kwa mwaka.

DIRA YA MKOA WA RUKWA.

Dira ya Mkoa ni “kuhakikisha kuwa huduma zote muhimu zinatolewa kwa wadau wote kwa wakati na kwa kiwango cha juu na kinachokubalika siku zote kwa ajili ya maisha bora na mazuri ili kuweza kuondokana na umaskini uliokithiri ifikapo mwaka 2025”.

 

VIPAUMBELE VYA MKOA.

Katika kutekeleza Ilani ya Uchaguzi na MKUKUTA na kwa kuzingatia Jiografia, majukumu na malengo ya Mkoa yamejikita katika kutekeleza vipaumbele vifuatavyo: Kuboresha Miundombinu, Kilimo, Elimu, Maendeleo ya Watumishi, Mazingira, Maji, Huduma za Afya, Mapambano dhidi ya UKIMWI na kuhamasisha uanzishaji wa SACCOS.

 

 MAFANIKIO YA MKOA WA RUKWA KWA MUDA WA MIAKA 50 YA UHURU.

Katika kipindi cha miaka 50 ya Uhuru Mkoa wa Rukwa umeendelea kutekeleza majukumu mbalimbali katika kupambana na Umaskini, Ujinga na Maradhi. Kwa kipindi chote cha Miaka 50 ya Uhuru Mkoa wa Rukwa umepata mafanikio makubwa ya Maendeleo katika nyanja za Kiuchumi, Kijamii, na Kisiasa. Baadhi ya Mafanikio hayo ni kuanzishwa kwa Mkoa Mpya wa Rukwa mwaka 1974, kuanzishwa kwa Wilaya tatu za Mpanda, Nkasi na Sumbawanga pamoja na uanzishwaji wa Halmashauri tano ambazo ni Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi, Mpanda, Sumbawanga na Halmashauri ya Mji Mpanda na Manispaa ya Sumbawanga pia mwezi Juni 2010 Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alitangaza kuanzishwa kwa Mkoa Mpya wa Katavi na Wilaya ya Mlele.

 

2.0     MAFANIKIO YA MKOA YA MIAKA 50 YA UHURU KWA KILA SEKTA.

2.1        KILIMO

Mkoa wa Rukwa katika kipindi cha Miaka 50 ya Uhuru wa Tanzania umeendelea kutekeleza na kubuni Mikakati mbalimbali ili kuinua sekta ya Kilimo. Mafanikio yafuatayo yamepatikana kutokana na juhudi hizo.

·         Wakati mkoa wa Rukwa unaanzishwa mwaka 1974 hapakuwepo na mwongozo mahsusi ulioandaliwa na mkoa kwa ajili ya kuendeleza Sekta ya Kilimo lakini mwaka 2008 Mkoa wa Rukwa umefanikiwa kubuni Mwongozo (mpango) wake unaojulikana kama Mkakati wa Mapinduzi ya Kilimo Rukwa (MAKIRU) kwa ajili ya Sekta hii. Mwongozo huu umewezesha Mkoa kutafsiri Mikakati ya kitaifa kama ‘Kilimo Kwanza’ kulingana na fursa zake pamoja na vipaumbele vilivyokubalika kimkoa.

·         Kuanzia mwaka 1961 hadi mwaka 2000 bajeti ya maendeleo ya Sekta ya Kilimo iliyokuwa inatolewa ilikuwa kidogo isiyoweza kuendeleza na kuinua sekta ya Kilimo lakini katika bajeti ya mwaka 2010/11 bajeti ya sekta ya kilimo imeongezeka kufikia Sh 7,501,889,895/=.

·         Eneo linalolimwa mazao ya biashara limeongezeka kutoka hekta 2,188 mwaka 1961 hadi hekta 109,388.7 mwaka 2011.

·         Uzalishaji wa mazao mbalimbali ya chakula umeongezeka kutoka tani 39,397 mwaka 1961 hadi 1,969,873.8 mwaka 2010.

·         Uzalishaji wa mazao ya biashara umeongezeka kutoka tani 5,381 mwaka 1961 hadi tani 269,057.1 mwaka 2010.

·         Matumizi ya mbolea yameongezeka kutoka tani 372.9 mwaka 1961 hadi tani 18,644.5 mwaka 2011.

·         Mbolea ya ruzuku imeongezeka kutoka tani 268 mwaka 2005 hadi tani  13,400 mwaka 2011.

·         Matumizi ya wanyamakazi (maksai) katika kilimo yameongezeka kutoka 5% mwaka 1961 hadi 70% mwaka 2011.

·         Matumizi ya mbegu bora yameongezeka kutoka tani 81 mwaka 2005 hadi tani 4,025.5 mwaka 2011ukilinganisha na hali ilivyokuwa wakati mkoa unaanza ambapo wakulima walitumia mbegu asilia tu.

·         Matumizi ya matrekta madogo yameongezeka toka 0 mwaka 1961 hadi 225 mwaka 2011.

·         Matumizi ya matrekta makubwa yameongezeka kutoka matrekta 1 mwaka 1961 hadi matrekta 85 mwaka 2011.

·         Kilimo cha umwagiliaji kimeongezeka kutoka hekta 543 mwaka 2000 hadi hekta 27,136 mwaka 2011 ukilinganisha na hali ilivyokuwa wakati mkoa unaanza ambapo wakulima walilima kwa kutegemea majira ya mvua tu.

 

2.1.2 MIFUGO

MAFANIKIO – 1961 HADI 2011.

·         Majosho yanayofanya kazi yameongezeka kutoka 0 mwaka 1961 hadi  36 mwaka 2011.

·         Wataalam wa uhamilishaji (Artificial Insemination) wameongezeka kutoka 0 mwaka 1961 hadi 18 mwaka 2011 (wakijumuishwa wafugaji 6).

·         Madume bora yameongezeka kutoka 4 kwa mwaka 1961 hadi 210 mwaka 2011.

·         Idadi ya ng’ombe waliohamilishwa imeongezeka kutoka 7 mwaka 1961 hadi 363 mwaka 2011.

·         Dawa za kuogesha mifugo zenye ruzuku ya Serikali zimeongezeka kutoka lita   0 mwaka 2006 hadi lita 39,426.75 mwaka 2011. Ambapo mwanzo serikali haikuwa na mpango wa kutoa ruzuku kwa ajili pembejeo za kilimo.

·         Elimu kupitia mashamba darasa ya ufugaji imeongezeka kutoka 0 mwaka 1961 hadi mashamba darasa 62 mwaka 2011.

·         Malambo ya maji ya kunywesha mifugo yameongezeka kutoka 0 mwaka 1961 hadi 2 yaliyoko katika hatua za ujenzi mwaka 2011.

·         Idadi ya wafugaji waliopata mafunzo ya ufugaji bora imeongezeka kutoka 0 mwaka 1961 hadi 8411 mwaka 2011.

·         Mbuzi wa Maziwa wameongezeka kutoka 16 mwaka 1961 hadi 791 mwaka 2011.

·         Ng’ombe wa maziwa wameongezeka kutoka 136 mwaka 1961 hadi 6,797 mwaka 2011.

·         Utengaji wa maeneo ya malisho ya mifugo umeongezeka kutoka vijiji 0 mwaka 1961 hadi vijiji 73 mwaka 2011.

 

 2.1.3   UVUVI

MAFANIKIO – 1961 HADI 2011.

·         Matumizi ya zana bora za uvuvi yameongezeka kutoka injini za boati 20 mwaka 1961 hadi injini za boti 1024 mwaka 2011.

·         Katika kuwasaidia wavuvi kutumia maarifa ya kisasa ya uvuvi, waliopatiwa elimu ni 0 mwaka 1961 hadi 15,016 mwaka 2011. 

·         Katika jitihada za kupambana na uvuvi haramu idadi ya zana haramu zilizokamatwa na kuteketezwa zimeongezeka kutoka zana haramu 0 mwaka 1961 hadi 1484 mwaka 2011.

·         Mkoa umeunda kikosi kazi cha watu 12 kwa ajili ya kuinua sekta ya uvuvi mwaka 2011.

·         Ufugaji wa samaki umehamasishwa kwa kuanzisha mabwawa ya kufugia samaki 0 mwaka 1961 hadi 700 mwaka 2011.

 

2.1.4  USHIRIKA /SACCOS.

MAFANIKIO – 1961 HADI 2011.

·         Idadi ya vyama vya Ushirika vya Akiba na Mikopo (SACCOS) imeongezeka kutoka vyama 0  mwaka 1961 hadi 105 mwaka 2011.

·          Mtaji umeongezeka kutoka 0 mwaka 1961 hadi kufikia sh. 2,301,203,127/= mwaka 2011.

·         Aina nyingine za vyama vya ushirika vimeongezeka kutoka 0 mwaka 1961 hadi 29 mwaka 2011 ikiwa ni ongezeko la asilimia 100 na mtaji wa vyama hivi umefikia sh. 95,664,500/=. 

·         Katika kipindi cha miaka 50 ya Uhuru SACCOS za Rukwa zimepata jumla ya mikopo yenye thamani ya Sh. 6,101,992,400/= na jumla ya Sh. 3,572,981,541/= zimerejeshwa sawa na asilimia 59.4 ya mikopo iliyotolewa.

·         Tumekwisha anza mchakato wa kuanzisha Benki ya wananchi wa Mkoa wa Rukwa (Rukwa Community Bank ‘RCB’).

 

2.1.5    MAZINGIRA.

  MAFANIKIO – 1961 HADI 2011.

·         Uhifadhi wa vyanzo vya maji umeongezeka kutoka vyanzo 0 mwaka 1961 hadi 86 mwaka 2011.

·         Matumizi ya mizinga ya kisasa ya nyuki yameongezeka kutoka mizinga 0  mwaka 1961 hadi  5566 mwaka 2011.

·         Mipaka ya vijiji vyote 379 (100%) vya Mkoa imeshapimwa; vijiji 44 vimeandaa matumizi bora ya ardhi.

·         Hadi mwaka 2011 jumla ya miti 19,069,983 ilikuwa imepandwa.

·         Halmashauri zote zimetunga sheria ndogo za kudhibiti mazingira.

·         Mkoa umezuia uingizaji wa mifugo mipya Mkoani.

 

3.1  ELIMU

(i)    ELIMU YA AWALI:

Madarasa ya elimu ya awali yameongezeka kutoka 0 mwaka 1961 hadi 844 (2011).

 

(ii)       ELIMU YA MSINGI:

·         Asilimia ya uandikishaji darasa la kwanza imeongezeka kutoka chini ya asilimia 100 mwaka 1961 hadi asilimia 123.84 (2011).

·         Idadi ya Wanafunzi darasa la I – VII imeongezeka kutoka 5,968 (mwaka 1961 hadi 298,408 (2011).

·         Idadi ya shule za Msingi imeongezeka kutoka 10 mwaka 1961 hadi 508 (2011) ongezeko 5,080% zikiwemo shule 2 zisizo za serikali.

·         Idadi ya walimu imeongezeka kutoka 97 mwaka 1961 hadi 4840 (2011).

·         Idadi ya nyumba za walimu imeongezeka kutoka 42 mwaka 1961 hadi 2089 (2011).

·         Uwiano wa Kitabu kwa mwanafunzi (Book Pupil Ratio) umepungua na kufikia 1:3 na 1:4 hivi sasa.

·         Idadi ya wanafunzi wanaochaguliwa kuingia kidato cha kwanza imeongezeka kutoka 73 mwaka 1961 hadi 3,672 (2011

 

(iii)   ELIMU YA SEKONDARI:

·         Idadi ya shule za Sekondari za Serikali imeongezeka kutoka 0 mwaka 1961 hadi 99 mwaka 2011.

·         Idadi ya shule zisizo za Serikali imeongezeka kutoka 0 mwaka 1961 hadi 15 mwaka 2011.

·         Shule za Sekondari za Serikali zenye “A Level” zimeongezeka kutoka 0 mwaka 1961 hadi 8 mwaka 2011.

·         Shule za Sekondari zisizo za Serikali zenye “A Level” zimeongezeka kutoka 0 mwaka 1961 hadi 4 mwaka 2011.

·         Idadi ya wanafunzi imeongezeka kutoka 734 mwaka 1961 hadi 36,706 mwaka 2011.

·         Idadi ya walimu imeongezeka kutoka 20 mwaka 1961 hadi 995 (2011).

·         Hivi sasa Kata 86 kati ya 88 sawa na asilimia 97.7 zina shule za sekondari.

 

(iv)  ELIMU YA UALIMU:

Idadi ya Vyuo vya Ualimu imeongezeka kutoka 0 mwaka 1961 hadi 2 (2011) ongezeko la 100% baada ya kusajiliwa Chuo kisicho cha serikali cha Rukwa.

(v)    ELIMU YA UFUNDI:

Mkoa unavyo vituo vya Ufundi Stadi 6 katika Shule za Msingi na Vyuo vya Ufundi 3 vinavyotoa mafunzo ya Ufundi katika fani za useremala, uashi, ufundi chuma, ufundi magari, uchomeleaji, kompyuta na Sayansi Kimu.

(vi).        ELIMU YA JUU:

Mkoa unatawi la Chuo Kikuu Huria cha Tanzania kilichoanzishwa mwaka 2003 mpaka mwaka 2011 kuna vituo viwili vya Chuo hiki, kituo kimoja kipo Mpanda na kingine Sumbawanga.

 

3.2  AFYA:

MAFANIKIO – 1961 HADI 2011.

·         Zahanati zimeongezeka kutoka 4 mwaka 1961 hadi 224 mwaka 2011.

·         Vituo vya Afya vimeongezeka kutoka 0 mwaka 1961 hadi 34 mwaka 2011.

·         Hospitali zimeongezeka kutoka 1 mwaka 1961  hadi 4 mwaka 2011.

·         Mahudhurio ya kwanza chini ya wiki 16 ya mama wajawazito yameongezeka kutoka 0 mwaka 1961 hadi 54% (2011).

·         Kiwango cha mama wajawazito wanaojifungulia katika vituo vya kutolea huduma za Afya na kuhudumiwa na wahudumu wenye mafunzo kimeongezeka kutoka 0 mwaka 1961 hadi asilimia 58 (2010).

·         Vifo vya wazazi vimepungua kutoka 220/100,000 mpaka 134/100,000 (2010).

·         Utapiamlo mkali umepungua kutoka asilimia 8 hadi asilimia 1 (2011).

·         Chanjo ya watoto chini ya mwaka mmoja imeendelea kupata mafanikio kama ifuatavyo;

o   Polio (kutoka 93.2% hadi 101% (2011).

o   BCG (kutoka 92.7% hadi 102% (2011).

o   DPT HB3 (kutoka 90% hadi 92% (2011).

o   Measles (kutoka 95% hadi 122% (2011).

o   Pepopunda kwa wajawazito kutoka 80.5% hadi 109% (2011).

·         Kumekuwepo na vituo vya kutolea tiba kwa wazee katika Hospitali na vituo vya Afya mpaka kufikia Machi 2011 jumla ya wazee 14, 585 wamepata vitambulisho vya matibabu.

·         Vifo vya watoto wachanga (IMR) chini ya mwaka mmoja vimepungua kutoka 106/1000 hadi 87/1000 mwaka 2011.

·         Vifo vya watoto chini ya miaka mitano vimepungua kutoka 175/1000 hadi 122/1000 mwaka 2011.

·         Serikali katika kuboresha huduma kwa watumishi wake imeanza mpango wa kuboresha mazingira ya kufanyia kazi kwa kujenga nyumba 10 za watumishi katika kila Halmashauri. Mpango huu utasimamiwa na shirika la Benjamin Mkapa kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii.

·         Mkoa una Chuo cha Wauguzi kinachoendeshwa na Kanisa Katoliki Jimbo la Sumbawanga kilichopo Wilaya ya Nkasi Mjini Namanyere ambacho kimetoa wahitimu wa kwanza 24 mwaka 2007, 42 mwaka 2008 na 84 mwaka 2009.  Aidha, Mkoa una Chuo cha Waganga Wasaidizi Vijijini (RMA) katika Manispaa ya Sumbawanga na unategemea kufungua kingine katika Wilaya ya Mpanda mwishoni mwa mwaka huu wa 2011.

·         Umefanyika ukarabati wa Hospitali ya Mkoa kwa kipindi cha miaka mitatu mfululizo kuanzia mwaka 2007/08 hadi 2009/10. Serikali imetoa jumla ya Sh.1.8 bilioni kwa ajili ya ukarabati wa majengo 7, ujenzi wa majengo 11 na ununuzi wa majenereta 2.

3.3  UKIMWI.

Tangu ugonjwa huu ugundulike Mkoani mwaka 1986, Serikali ya Mkoa imechukua jitihada mbalimbali kukabiliana na tatizo hilo.  Jitihada zilizochukuliwa na zinazoendelea kuchukuliwa ni pamoja na kutoa elimu ya kinga kwa wananchi ili kubadili tabia, matumizi ya  damu salama  na tiba ya kupunguza makali ya ukimwi inayotolewa kwa wagonjwa.

 

 

      MAFANIKIO – 1986 HADI 2011.

·         Kiwango cha maambukizi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto mkoani kimepungua kutoka asilimia 6.7 hadi 4.9% mwaka 2011.

·         Katika huduma ya kuzuia maambukizi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto (PMTCT) kuna ongezeko la vituo 66 vya kutolea huduma kutoka 38 hadi 104 mwaka 2011.

·         Vituo vya ushauri nasaha na upimaji wa hiari vimeongezeka kutoka 0 hadi 85 mwaka 2011.

·         Idadi ya wateja waliojitokeza kupima kwa hiari imeongezeka toka watu 782 hadi watu 240,000 mwaka 2011.

·         Asasi za kiraia 76 zinachangia kwa kiasi kikubwa kutoa huduma kwa wateja wa UKIMWI hasa katika huduma za majumbani kwa waathirika, watoto yatima na wanaoishi katika mazingira magumu. Hadi sasa watoto yatima na wanaoishi katika mazingira magumu zaidi ya 12,567 wametambuliwa na kupewa huduma.

·         Vituo vya tiba ya kupunguza makali ya ukimwi vimeongezeka kutoka 0 mwaka 1986 hadi 20 mwaka 2011.

·         Hali ya maambukizi ya Virusi vya UKIMWI kwa sasa kiwango kimeshuka kutoka asilimia 6 hadi 4.9% mwaka 2011 ikilinganishwa na asilimia 5.8 ya wastani wa kitaifa.  Halmashauri inayoongoza ni Manispaa ya Sumbawanga kwa asilimia 6.5 na Halmashauri yenye kiwango cha chini ni Nkasi yenye asilimia 3.1.

·         Wagonjwa wanaopata matibabu ya dawa za ARV wameongezeka kutoka 0 mwaka 1986 hadi 6,175 mwaka 2011.

 

3.4  MAJI.

Katika kipindi cha Miaka 50 ya Uhuru Mkoa umeendelea kusogeza huduma ya maji safi na salama karibu na sehemu wanazoishi wananchi.

 

3.5  MAFANIKIO MAJI.

 Katika kipindi cha miaka 50 ya Uhuru mkoa umeendelea kusogeza huduma ya maji safi na salama karibu na sehemu wanazoishi wananchi.

 

MAFANIKIO – 1961  HADI 2011.

·         Miradi ya maji ya kutega imeongezeka kutoka 0 kwa kipindi cha mwaka 1961 hadi kufikia 36 mwaka 2011.

·         Visima virefu na vifupi vyenye pampu vinavyofanya kazi vimeongezeka kutoka 22 kwa kipindi cha mwaka 1961  hadi 1079 mwaka 2011.

·         Idadi ya watu wanaopata huduma ya maji safi imeongezeka kutoka 0 mwaka 1961 hadi asilimia 50.5 mwaka 2011.

·         Mradi wa maendeleo ya sekta ya maji umeanza kutekelezwa ambapo katika Manispaa ya Sumbawanga kupitia Mamlaka ya Maji Safi na Maji taka ya Sumbawanga mkandarasi amekwisha anza kazi ya ukarabati wa mtandao wa maji na uchimbaji wa visima virefu unaendelea.

·         Halmashauri zetu zote Makandarasi washauri wamekamilisha zoezi la uandaaji wa taarifa ambazo zitasaidia katika kutekeleza mradi unaojulikana kwa jina la mradi wa vijiji 10 kwa kila Halmashauri.

Halmashauri zina kamati hai na mifuko ya maji 273 yenye jumla ya shilingi 83,257,180.91/= hadi 2011.

·         Halmashauri ya Mji Mpanda imejenga visima na matanki ya kusambazia maji kufikia wakazi wapatao 2000 katika Kata ya Nsemulwa, Majengo na Kawajense.

3.6  MIUNDOMBINU.

Mkoa wa Rukwa una mtandao wa barabara unaokadiriwa kuwa na kilomita 5,502.3. Mtandao wa barabara unaohudumiwa na Wizara ya Miundombinu kupitia Wakala wa Barabara (TANROADS) Mkoani Rukwa una jumla ya kilomita 2,150 ambapo Barabara Kuu ni kilomita 887 na barabara za Mkoa ni kilomita 1,263 mwaka 2011.

 

MAFANIKIO – 1961 HADI 2011.

Kwa muda wa Miaka 50 ya uhuru Mkoa wa Rukwa haukuunganishwa na mikoa mingine kwa kiwango cha lami na hivyo kufanya barabara za Mkoa kupitika kwa msimu. Lakini katika mwaka 2010/2011 Serikali imesaini mikataba mbalimbali kwa ajili ya kutengeza barabara za mkoa kwa kiwango cha lami mikataba hiyo ni:-

·         Mkataba wa ujenzi wa Barabara ya Tunduma-Laela-Sumbawanga kwa kiwango cha lami ambapo hivi sasa ujenzi unaendelea. Barabara hii imegawanywa katika sehemu tatu ili kuharakisha ujenzi (Tunduma-Ikana km.64; Ikana-Laela km.64 na Laela-Sumbawanga km.96.5).

·         Mkataba wa ujenzi wa barabara ya Laela-Sumbawanga (96.5 km) kwa kiwango cha lami ulisainiwa tarehe 29/04/2010 ambapo jina la Mkandarasi ni AARSLEEF-BAM International JV kutoka nchini Denmark na Uholanzi. Tarehe 11/06/2010 Mkandarasi alikabidhiwa rasmi barabara hiyo, barabara hii mpaka kukamilika itaghalimu USD 97 Milion. Maendeleo ya jumla ya mradi hadi kufikia tarehe 31Machi 2011 yalikuwa yamefikia 9% ya kazi zote zilizopangwa, kwa ujumla mradi unaendelea vizuri.

·         Mkataba wa ujenzi wa barabara ya Ikana-Laela (64.2 km) kwa kiwango cha lami ulisainiwa tarehe 17/09/2010 ambapo jina la Mkandarasi ni China New Era International Enginering Corporation kutoka nchini China na Kampuni ya Ushauri ya Kihandisi iitwayo Egis BCEOM kutoka Ufaransa. Gharama za ukamilishaji wa mradi huu ni Sh. 76.1 Bilion, maendeleo ya mradi hadi Machi, 31 2011Mkandarasi alikuwa anaendelea na maandalizi ya kuanza kazi ikiwa ni pamoja na ujenzi wa kambi katika kijiji cha Myunga Wilayani Mbozi, pia amekamilisha usimikaji wa mtambo wa kusaga kokoto (crusher) kwa ujumla Mkandarasi huyu amefanya maandalizi makubwa kwa muda mfupi.

·         Mkataba wa ujenzi wa barabara ya Tunduma - Ikana (63.7 km) kwa kiwango cha lami ulisainiwa tarehe 22/09/2010 ambapo jina la Mkandarasi ni Consolidated Contractors Group S.A (offshore)(CCC) kutoka nchini Ugriki na Egis BCEOM International kutoka Ufaransa, barabara hii mpaka kukamilika itaghalimu Sh. 82.5 Bilion. Maendeleo ya mradi hadi kufikia tarehe 31 Machi 2011 Mkandarasi alikuwa anaendelea na maandalizi ya kuanza kazi ikiwa ni pamoja na ujenzi wa kambi katika kijiji cha Chipaka Wilayani Mbozi.

 

·         Barabara ya Sumbawanga-Chala-Kanazi (Namanyere) yenye urefu wa km.75 inajengwa na Mkandarasi aitwaye Jiangxi Geo-Engineering Group Corporation kwa gharama ya Shilingi 78,840,000,000/=, mkataba huu ulisainiwa tarehe 15/06/2009. Maendeleo ya jumla ya mradi huu kufikia 31Machi 2011 yalikuwa 9.4% ya kazi zote zilizopangwa kuchelewa kwa malipo ya Mkandarasi kumechangia utekelezaji wa mradi kuwa na kasi ndogo.

·         Barabara ya Kanazi (Namanyere)-Kizi-Kibaoni yenye urefu wa km.76 inajengwa na Mkandarasi aitwaye China Hunan Construction Engineering Group Corporation kwa gharama ya Shilingi 82,840,000,000/= mkataba ulisainiwa tarehe 15/07/2009, Maendeleo ya mradi huu hadi kufikia tarehe 31 Machi 2011 yalikuwa 17% ya kazi zote zilizopangwa. Mkandarasi anaendelea vizuri ingawa kuchelewa kwa malipo ya Mkandarasi kumeathiri kasi ya utekelezaji wa mradi.

·         Mkataba wa ujenzi wa Barabara ya Sumbawanga-Matai-Kasanga yenye urefu wa km.112 kwa kiwango cha lami ulisainiwa tarehe 7 Oktoba 2009.  Mkandarasi aliyepewa kazi hii ni China Railway 15 Bureau Group Corporation (CR15G) akishirikiana na Henan Provincial Newcentry Road & Bridge Consultants Ltd ambapo gharama za ujenzi ni Shilingi 133,287,000,000/=.  Mradi umepangwa kukamilika katika kipindi cha miaka mitatu (3).  Barabara hii itajengwa kwa mkataba wa kufanya usanifu na kujenga (Design and Build Contract).  Maendeleo ya mradi hu hadi kufikia 31 Machi 2011 yalikuwa 5.11% ya kazi zote zilizopangwa mradi huu unatekelezwa na mkataba wa usanifu wa ujenzi (Design and Build Contract). Usanifu wa kina wa kilometa 70 za kwanza umekamilika na Mkandarasi ameruhusiwa kuanza kazi kaika kilometa 20 za kwanza. Usanifu wa kilometa 42 zilizobaki unaendelea.

·         Upembuzi Yakinifu na Usanifu wa Kina (Feasibility Study and Detailed Engineering Design) kwa barabara ya Mpanda-Uvinza-Kanyani (Kasulu) yenye urefu wa km.252 unaendelea vizuri. Kazi ya upembuzi yakinifu imekamilika na Kazi ya usanifu wa kina inayofanywa na Kampuni ya Crown Tech-Consult ya Dar es Salaam iko katika hatua za mwisho.

 

·         Upembuzi Yakinifu, Usanifu wa Kina na kuandaa Nyaraka za Zabuni (Feasibility Study, Detailed Engineering Design and Preparation of Tender Documents) kwa barabara ya Mpanda-Koga-Tabora yenye urefu wa km.359 unaendelea vizuri kwani kazi ya Upembuzi Yakinifu, Usanifu wa kina na kuandaa nyaraka za zabuni kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya Mpanda-Koga-Tabora kwa kiwango cha lami inayofanywa na Kampuni ya COWI A/S kutoka Denmark na COWI Tanzania inaendelea.

·         Ukarabati na Matengenezo ya Barabara Kuu na za Mkoa kupitia mpango wa PMMR (Performance Based Management and Maintenance of Roads) km.363.78 kwa gharama ya Shilingi 8,438,063,163.02 unaendelea vizuri.  Tumeomba barabara zingine ziingizwe katika mpango huu ili kufidia kilomita zilizoingizwa kwenye ujenzi wa barabara ya Sumbawanga-Namanyere-Mpanda kwa kiwango cha lami.  Aidha tumeziagiza Halmashauri zetu zijifunze kuhusu utekelezaji wa PMMR ili kama utawafaa wauige katika ukarabati wa barabara na utoaji wa huduma mbalimbali.

·         Wakati mkoa unaanza hakukuwepo na simu za mkononi. Ilipofikia mwaka 2005, mtandao wa simu za mkononi ulikuwa unapatikana Makao Makuu ya Wilaya tu. Leo, 2011, simu za mkononi zinapatikana karibu Mkoa mzima wa Rukwa hadi maeneo ya mipakani mwa Chunya (Mbeya), Mishamo karibu na Kigoma na mpakani mwa Zambia.

·         Kiwanja cha Ndege cha Mpanda kimeboreshwa na sasa kinajengwa kwa kiwango cha lami.

 

3.7  WATUMISHI.

Kwa muda wa miaka 50 ya Uhuru mkoa umekuwa na upungufu wa watumishi katika sekta zote. Ili kupata watumishi wa kutosha jitihada mbalimbali zimefanyika ikiwa ni pamoja na:-

·         Kuanzisha na kusajili “Mfuko wa Kuboresha Mazingira ya Watumishi” mwaka 2006 ili kuvutia watumishi wanaopangwa kufanya kazi mkoani Rukwa, kwa kutoa vivutio kwa watumishi wanaokubali kuja kufanya kazi Rukwa. Halmashauri zote zinachangia mfuko huu kila mwaka, ambao umesaidia sana kupunguza tatizo la walimu wa Sekondari na watumishi wa sekta ya Afya. Hadi tarehe 08/04/2011 mfuko ulikuwa na jumla ya Sh. 7,115,437.53 kwenye akaunti zake mbili zilizo katika benki za CRDB na NMB na uwekezaji kiasi cha Sh. 200 million katika Mfuko wa Umoja ili kukuza mtaji wake na kuwa endelevu.

·         Mkoa umeendelea kupanua na kuboresha elimu ya Sekondari ili kupata vijana wengi wa Mkoa huu ambao tunaamini haitakuwa kikwazo kwao kufanya kazi Rukwa.

·         Mkoa umeendelea kutoa mafunzo ya muda mfupi na muda mrefu kwa watumishi ili kuwaendeleza watumishi waliopo.

·         Mwaka 1961 walikuwepo watumishi wachache waliokuwa wamesoma na wasiokuwa na ujuzi wa kutosha, suala la kuwaendeleza watumishi limeanza miaka ya 2007 hadi mwaka 2011 ambapo Sekretarieti ya Mkoa imepeleka masomoni watumishi 78 kuanzia ngazi ya cheti hadi shahada ya pili.

 

3.8  HALI YA UWEKEZAJI MKOA WA RUKWA.

Hali ya Uwekezaji katika Mkoa wa Rukwa kuanzia mwaka 1961 hadi mwaka 2000 haikuwa nzuri, lakini kuanzia mwaka 2000 hadi 2011 Mkoa unafanya vizuri katika uwekezaji, kwa kuzinadi fursa mbalimbali zilizopo, baada ya Warsha ya Uwekezaji ya Juni 2007 Wawekezaji walioitikia wito wa kuwekeza Mkoani Rukwa ni:-

1. Mikebuka Fisheries Ltd. - Kununua na kusafirisha samaki.

2. Energy Milling Ltd.           -Usindikaji nafaka hususani mahindi na mpunga.

3. Malonje Heritage Farm - Ufugaji ng’ombe wa maziwa na usindikaji bidhaa za maziwa.

4. Brand International Ltd - Uchimbaji wa Madini ya risasi- Mpanda.

5.Barka Milling    -Kusindika nafaka Malangali–Sumbawanga(ujenzi unaendelea).        

6. Executive Lodges             - Hoteli – Sumbawanga.

7. Katavi Hippopotamus     - Hoteli Sitalike – Mpanda.

8. Katavi Tented Hotels        - Camp site Katavi – Mpanda.

9. Blue Water Tanzania LTD -Kiwanda cha Maji Sumbawanga (ujenzi unaendelea).

10. Lake shore Lodge & Campsite - Hoteli ya kitalii Kipili Nkasi.

11. SAAFI MEAT Ltd. Co  - Kiwanda cha kusindika nyama kilichopo Mjini Sumbawanga.

 

Wawekezaji Wengine.

 Wawekezaji walioonesha nia na waliofika kutembelea Mkoa wetu ni Kampuni ya ‘NO TILL’ kutoka Australia, Vetex Consultants (USA), Kiwanda cha Bia (TBL) na Agrisol (T) Ltd wanaotaka kuwekeza kwenye kilimo na usindikaji wa mazao ya kilimo. Wengine ni Tanzania Strategic Development Ltd kwa kushirikiana na Kampuni ya Upendo wanataka kuzalisha nishati ya umeme kwa kutumia makaa ya mawe na Indian Mining Co. wanaotaka kuwekeza kwenye uchimbaji Madini.

 

CHANGAMOTO KUU ZINAZOKABILI MKOA.

·         Mkoa una upungufu mkubwa wa watumishi katika sekta zote na wengi wao ni wale wenye ujuzi usiokidhi. Pia kutokana na utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi shule nyingi za sekondari na msingi zimejengwa. Kwa hali hii kuna upungufu mkubwa wa walimu, vifaa na samani.

·         Mkoa bado unakabiliwa na tatizo kubwa la upatikanaji wa umeme wa uhakika kwani kwa sasa makao makuu ya mkoa yanapata umeme kutoka nchi ya jirani ya Zambia, Namanyere na Mpanda zinatumia Jenereta.

·         Kuwepo kwa miundombinu mibovu hususan barabara katika maeneo mengi ya mkoa wa Rukwa na mawasiliano ya msimu ya anga kupitia viwanja vidogo vya ndege vya Sumbawanga na Mpanda.

·          Kutokuwepo kwa wawekezaji wa maendeleo kwa muda mrefu katika Mkoa wa Rukwa na hivyo kusababisha Maliasili kama ardí, madini na wanyama pori kutowanufaisha wananchi.

·         Mkoa unakabiliwa na kuwepo kwa gharama kubwa za matengenezo ya barabara, kutokana na kutokuwepo kwa Kituo cha Ukodishaji wa Mitambo ya Ujenzi katika Mkoa wa Rukwa (kama ilivyo Mbeya).

 

7. MIPANGO YA  KUKABILIANA NA CHANGAMOTO.

·         Mkoa utaendelea kupanua na kuboresha elimu ya ngazi zote ili kupata vijana wengi wa mkoa huu ambao tunaamini haitakuwa kikwazo kwao kufanyakazi Rukwa.

·         Kuimarisha mfuko wa kuboresha mazingira ya watumishi ili uweze kutoa huduma kwa sekta zote kwa kuwavutia watumishi wengi zaidi.

·         Kuendelea kushawishi serikali na wawekezaji wengine kuwekeza katika upatikanaji wa umeme wa uhakika mkoani.

·         Mipango iliyopo ni kutengenezwa kwa kiwango cha lami barabara kuu tatu za Tunduma – Sumbawanga, Sumbawanga- Kasanga na Sumbawanga – Namanyere - Kibaoni - Mpanda. Pia viwanja vidogo vya ndege vya Sumbawanga na Mpanda vinakarabatiwa ili viweze kutoa huduma ya usafiri wa anga kwa mwaka mzima.

·         Mkoa unaendelea kushawishi wawekezaji kuja kuwekeza na wanaendelea kujitokeza.

·         Kuna mchakato wa ujenzi wa Chuo Kikuu cha Kilimo Wilayani Mpanda ili kuweza kuongeza wigo wa wataalam wa kilimo na kutoa nafasi ya ajira kwa wakazi wa mkoa wa Rukwa na Tanzania kwa ujumla.