MAPINDUZI YA KILIMO RUKWA (MAKIRU)
AWAMU YA KWANZA
2008/2009 HADI 2010/2011
1.0 UTANGULIZI
Mkoa wa Rukwa ni miongoni mwa mikoa 21 ya Tanzania bara. Mkoa wa Rukwa kijografia upo kusini magharibi ya Tanzania na unapakana na nchi za Zambia na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Rukwa ni kati ya mikoa mashuhuri minne ya Nyanda za Juu Kusini ‘ The Big Four' katika uzalishaji wa mazao ya nafaka hasa mahindi, mpunga na ulezi .
Mkoa wa Rukwa una hali ya hewa nzuri inayofaa kwa kilimo na ufugaji. Kilimo na ufugaji unaofanywa na wakulima wadogo wadogo wa mkoa huu hauna tija kwa sababu wakulima na wafugaji wetu wana kiwango kidogo cha elimu ya kilimo/ufugaji, matumizi kidogo ya pembejeo na zana duni za kilimo, kilimo kinachotegemea mvua tu na hawana malengo ya kibiashara. Pamoja na kwamba Mkoa wa Rukwa una mazingira mazuri kwa uzalishaji wa mazao ya kilimo na ufugaji na kuwa miongoni mwa mikoa minne inayozalisha mazao ya nafaka kwa wingi nchini, lakini bado hali ya uzalishaji kwa eneo ipo chini. Kwa mfano, wastani wa uzalishaji kwa hekta wa zao la mahindi ni tani 2 tu, mpunga ni tani 3, alizeti ni tani 1.2 tu; badala ya tani 5 hadi 6 kwa mahindi, tani 5.6 kwa mpunga na 2.5 kwa alizeti. Fursa zilizopo hazijatumika kikamilifu kukiendeleza kilimo na ufugaji kwa manufaa ya wakazi wa Mkoa wa Rukwa na Taifa kwa ujumla.
Pamoja na hayo uzalishaji unaopatikana bado unakumbwa na tatizo kubwa la usafiri na usafirishaji kutoka mashambani kwenda sokoni kwa ajili ya walaji wa ndani na nje. Miundombinu kwa sehemu kubwa katika mkoa huu ni duni. Jumla ya kilomita 4,987 za mtandao wa barabara ni za udongo zisizopitika vizuri wakati wa masika. Kutokana na ubovu wa miundombinu, pembejeo kwa ajili ya kilimo zinakuwa ghali sababu ya gharama za usafirishaji na ufikishaji mazao sokoni inakuwa tatizo, hivyo kupata bei ndogo. Aidha, mkoa hauna viwanda vya kutosha kusindika mazao mbalimbali yanayozalishwa mkoani ili kuyaongezea thamani na kuwa soko la uhakika kwa mazao ya wakulima.
Kwa kubaini matatizo hayo, Serikali ya Mkoa wa Rukwa kwa kushirikiana na Halmashauri na wadau mbalimbali imeazimia kuleta Mapinduzi ya Kilimo kwa kuandaa Mpango Mkakati wa Mapinduzi ya Kilimo Rukwa (MAKIRU) . Tunakusudia kuelekeza rasilimali na nguvu zetu na wadau mbalimbali katika kuwasaidia na kuwaunganisha wakulima/wafugaji katika kulima kilimo na ufugaji wenye tija ili waondokane na umaskini. Kazi kubwa ambayo tunatarajia kuifanya ni pamoja na kuwaelimisha wananchi wakione kilimo na mifugo kuwa ni biashara wala siyo kwa ajili ya chakula chao tu. Watumie utaalamu na pembejeo kuwezesha kufikia kiasi cha juu cha uzalishaji kinachoweza kufikiwa, kulima kulingana na mahitaji ya soko na kusindika mazao ili kuyaongezea thamani.
Mkoa wa Rukwa una ardhi nzuri yenye rutuba ya asili inayofaa kwa kilimo na ufugaji yenye ukubwa wa eneo la hekta 2, 357, 029. Eneo linalolimwa kwa sasa ni hekta 598,176 sawa na asilimia 25 tu ya eneo lote linalofaa kwa kilimo. Mkoa una hali ya hewa nzuri na mvua za kuaminika kati ya milimita 750 na 1,000 kwa mwaka zinazofaa kwa uzalishaji wa mazao mengi. Aidha, unayo mabonde ya mito yenye jumla ya ukubwa wa hekta 172,295 yanayofaa kwa kilimo cha umwagiliaji; eneo linalitumika kwa kilimo cha umwagiliaji kwa sasa ni hekta 21,117.7 sawa na asilimia 12.26 ya eneo lote linalofaa kwa kilimo cha umwagiliaji. Pamoja na fursa hizo zote, Mkoa wa Rukwa bado unaendelea na kilimo kisicho na tija kwa Mkulima wala kisichoendana na dunia hii ya karne ya 21 ya sayansi na teknolojia.
Changamoto kubwa zinazokwamisha kukua kwa sekta ya kilimo katika Mkoa wa Rukwa na kuwa na tija ndogo katika uzalishaji wa mazao ya kilimo na mifugo ni kama zifuatavyo:
Matumizi kidogo ya pembejeo na zana duni za kilimo,
Elimu na stadi za wakulima/wafugaji kwa uzalishaji ni ndogo
Matumizi madogo ya fursa kubwa ya umwagiliaji iliyopo
katika mkoa.
Miundombinu duni katika maeneo yenye fursa kubwa ya
uzalishaji
Uwezo mdogo wa kusindika mazao mbalimbali na kuyaongezea thamani.
Ukosefu wa mitaji, pamoja na kutokuwepo kwa taarifa za
kutosha kwa wakulima kuhusiana na taasisi za kifedha mikopo/ misaada
Ukosefu wa mfumo wa taarifa za masoko.
Udhaifu wa mfumo wa mawasiliano (linkage) katika usambazaji wa teknolojia toka vituo vya utafiti kwenda Halmashauri hadi kwa wananchi,
Kuwepo kwa upotevu mkubwa wa mazao shambani na
Ghalani, na
Kukosa uwekezaji katika kilimo cha mashamba makubwa ya kibiashara
2 MADHUMUNI YA MPANGO MKAKATI WA MAKIRU
Mkoa wa Rukwa una jukumu kubwa la kitaifa kutumia fursa nyingi zilizopo na kuondoa vikwazo vilivyopo ili kufanya Mpango Maalumu utakaoleta Mapinduzi ya Kilimo kwa muda mfupi. Mapinduzi yatakayoongeza uzalishaji, tija na kipato kwa wakulima kwa njia ya Kilimo na ufugaji wa kisasa.
Madhumuni ya Mpango Mkakati huu ni kuzalisha mazao ya kilimo na mifugo kwa tija na kuuza ziada katika maeneo ya nchi yetu yatakayokuwa na upungufu wa chakula. Aidha, ziada nyingine ya chakula itauzwa nchi za nje na kukuza uchumi wa wananchi wetu na kuliingizia taifa fedha za kigeni.
Haja ya kuwa na Mapinduzi ya Kilimo mkoani Rukwa ni muhimu sana hasa kwa kuzingatia kuwa sekta ya kilimo ndiyo inayoajiri aslimia kubwa ya wakazi wake, zaidi ya asilimia 90, kilimo ndiyo chanzo kikuu cha uchumi wa wakazi wa Mkoa wa Rukwa kinachangia karibu asilimia 65 ya pato la Mkoa na fursa za kuendeleza kilimo na ufugaji ni nyingi lakini hazijatumiwa vya kutosha kumuondolea mwananchi umasikini.
Mazao makuu yanayostawishwa katika mkoa ni pamoja na Mahindi, Maharagwe, Mpunga, Mhogo, Ulezi, Karanga, Viazi vitamu, na Ngano. Aidha, mazao ya biashara ni Tumbaku, Alizeti, Kahawa na Ufuta. Zao la mahindi linalolimwa kwa wingi na kwa mtawanyiko mkubwa mkoani ndilo linalowapatia wananchi wengi fedha hasa baada ya Serikali kutupatia kibali cha kuuza nje ya nchi ziada ya mazao ya chakula. Linachangi karibu asilimia 35 ya pato la Mkoa.
Kikao cha kazi cha tarehe 03 Julai 2008 kilichofanyika katika ukumbi wa jengo la Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, uamuzi ulifikiwa wa kuunda kikundi kazi cha Wataalam ambacho kiliongozwa na Mwenyekiti wake Bw. T. Sijabaje Mkuu wa Wilaya ya Mpanda, na Katibu wake akiwa ni Bw. H. Mvano Mshauri wa Kilimo wa Sekretarieti ya Mkoa. Wajumbe wengine wa Kikundi kazi hicho ni pamoja na Bw. D.E.P Kilonzo Mshauri wa Mipango na Uchumi wa Sekretarieti ya Mkoa, Bw. O.S Magehema Afisa kilimo wa Halmashauri ya wilaya ya Mpanda, Dr. Malebeja Afisa mifugo wa wilaya ya Sumbawanga, Bw. Elikunda Afisa Mfawidhi wa kituo kidogo cha Utafiti Milundikwa, maafisa Ardhi, maafisa maendeleo ya jamii, Afisa Magereza. (Dr. Loum Mshuri wa mifugo wa sekretariet ya Mkoa na Bw. L.m Sesemkwa Mshauri wa Ushirika wa Sekrtarieti ya Mkoa.) Timu ilikuwa na jukumu kubwa la kuandaa Mpango Mkakati Maalumu wa Mkoa utakaohakikisha utekelezaji wa MAKIRU unaandaliwa na kuwasilishwa kwa Mkuu wa Mkoa wa Rukwa kabla ya tarehe 03 Agosti 2008, kutokana na sababu zilizokuwa nje ya uwezo wetu, Kikundi kazi hiki kilizinduliwa na Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mhe. Daniel Ole Njoolay na kuanza kazi huko Mpanda tarehe 11 Julai 2008, siku tisa baada ya kuteuliwa. Kutokana wa ugumu wa kazi katika utekelezaji wake, kazi hiyo inawasilishwa leo tarehe 18 Agosti 2008.
Katika kutekeleza kwa vitendo jukumu hili kubwa na zito, Serikali ya Mkoa chini ya uongozi wa Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Mheshimiwa Daniel Ole Njoolay imeandaa Mpango Mkakati wa MAKIRU wenye makusudio ya kuzijengea uwezo Halmashauri za Manispaa, Mji na Wilaya, Taasisi zinazojishughulisha na Kilimo zilizoko Mkoani Rukwa, pamoja na wakulima wa Mkoa wa Rukwa kwa ujumla; na kutoa msukumo wa aina yake katika kuleta Mapinduzi ya Kilimo Mkoani Rukwa.
Mambo ya kupewa kipaumbele katika Mpango Mkakati wa MAKIRU yatakuwa kama ifuatavvyo:-
(i) Uangalifu mkubwa utawekwa katika kuhakikisha kuwa zana bora za kilimo zinapatikana na zilizopo (plau na matrekta) zinatumika vizuri ili ziweze kutoa matokeo yanayotarajiwa na kudumu kwa muda mrefu.
(ii) Uangalifu mkubwa utachukuliwa katika kuhakikisha kuwa, pembejeo za kilimo/mifugo (mbolea, mbegu bora, madawa) zinapatikana na zinatumika wakati wote kwa mujibu wa maelekezo na ushauri wa wataalam wetu wa Kilimona mifugo.
(iii) Kuhakikisha kuwa eneo dogo linatoa mazao mengi na bora.
(iv) Kila Halmashuri kuhakikisha kuwa Wataalam wa kilimo/mifugo waliopo wanapangwa vizuri ili kutoa utaalamu wao kwa wakulima/wafugaji vijijini.
|